Wednesday, May 1, 2013

MADOLA YA OKWI FIFA KUINGILIA KATI, TIRIRIKA...........

SHIRIKISHO la Soka la Kimataifa (Fifa) limemteua ofisa wake mmoja aanze kushughulikia suala la fedha zinazotokana na malipo ya mshambuliaji Emmanuel Okwi wanazotakiwa kulipwa Simba.
Ofisa huyo anayejulikana kwa jina la Mario Di Mangos ndiye atafanya kazi hiyo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia inailipa Simba dola 300,000 (zaidi ya Sh milioni 480).
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage amethibitisha kuhusiana na taarifa za Di Mango kupewa kazi hiyo na Fifa.
“Kweli, Di Mango ndiye atashughulikia suala hilo na Fifa wameahidi kuleta barua kuhusiana na uteuzi huo.
“Maana Etoile Du Sahel wanataka kuleta mambo ambayo si sahihi, wanasema kuna matatizo ya uhamishaji fedha sijui kuna masharti ya benki kuu yanawabana. Sisi tunaona si sahihi na tunataka fedha zetu,” alisema Rage.
Awali Simba ilikuwa imeteua wajumbe watatu kwa ajili ya kwenda Tunisia Mei 21 kwa ajili ya kufuatilia fedha hizo.
Etoile du Sahel iliahidi kuilipa Simba kitita cha dola 150,000 kama awamu ya kwanza na fedha hizo zilitarajiwa kutua nchini Januari 31 lakini mambo hayakuwa hivyo kama ilivyokuwa kwa awamu ya pili ambayo wangelipa Februari 28, mwaka huu.
Baada ya hapo, Simba imekuwa ikihaha kila kukicha kupata fedha hizo na mara kadhaa imekuwa ikikumbana na ukata na uongozi wa Rage umekuwa ukilalama kwamba unadai fedha nyingi kwa wadau mbalimbali zikiwemo hizo za Okwi.

No comments: