![]() |
| Add caption |
Kocha wa Stars, Kim Poulsen kushoto akipambana na askari wa Uwanja wa Marakech

Na Mahmlud Zubeiry, Marakech, IMEWEKWA JUNI 8, 2013 SAA 8:00 USIKUTIMU
ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars usiku huu imekiona cha moto
mbele ya askari wa Uwanja wa Marakech, baada ya kufanyiwa vurugu na
kuzimiwa taa ishindwe kufanya mazoezi kwenye Uwanja huo siku moja kabla
ya mchezo wao na wenyeji wao Morocco kesho, kuwania tiketi ya kucheza
Fainali za Kombe la Dunia. Sheria
za FIFA zinasema timu mgeni, itapewa fursa ya kufanya mazoezi katika
Uwanja utakaotumika kwa mechi dhidi ya wenyeji katika muda ambao mechi
itachezwa, lakini leo msafara wa Stars ulipofika Uwanja wa Marakech
ulizuiwa kuingia ndani na askari wa uwanjani hapo. Juhudi
za Kocha mkuu wa Stars, Kim Poulsen kuwaelewesha askari wa Uwanja huo
sheria ili wairuhusu timu kuingia uwanjani hazikuzaa matunda na ikabidi
viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) waingilie kati, nao pia
wakachemsha.

Wasiwasi; Kutoka kulia DK Dau, Mh Zitto Kabwe, Mh Mohamed Dewji na Magori wakijadiliana uwanjani

Wasiwasi; Kutoka kulia DK Dau, Mh Zitto Kabwe, Mh Mohamed Dewji na Magori wakijadiliana uwanjani
Ikawadia
zamu ya viongozi wa Kamati ya Ushindi ya Stars, inayodhaminiwa na
Kilimanjaro Premum Lager, ambao nao walichemsha- ndipo baadhi wa
Watanzania waishio hapa na wachache waliosafiri kutoka Dar es Salaam
walipoongeza nguvu.Walikwenda kufungua geti kwa nguvu, wakawaweka kando askari waliokuwa wanawazuia na kuiingiza timu uwanjani kufanya mazoezi. Hata hivyo, Stars ilipofika uwanjani ililazimika kusubiri tena, kwani wenyeji Simba wa Atlasi walikuwa wakiendelea na mazoezi.Baada
ya nusu saa, Morocco walimaliza awamu yao na Stars wakaanza kupasha
misuli moto. Hata hivyo, baada ya dakika 34, taa za Uwanja huo zilizimwa
na uwanjani kuwa giza totoro, lakini viongozi wa TFF wakaenda kuomba,
zikawashwa na timu ikafanya mazoezi kwa dakika 10 zaidi. Naibu
Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Mh. Amos Makalla aliyekuwapo
wakati wa vurumai zote hizo, alisikitishwa mno na kitendo hicho akisema
si cha kiungwana na si cha kiunamichezo.

Makamu wa Rais wa TFF, Athumani Nyamlani alisema Morocco walikuja kucheza Dar es Salaam walipokewa vizuri na wakahudumiwa vizuri hadi wanaondoka, ajabu leo wanaifanyia ‘unyama’ Tanzania.Mkuu wa Msafara wa Stars hapa, Crescentius John Magori alisema watapeleka malalamiko FIFA, waandaji wa michuano ya kufuzu kwa Kombe la Dunia na kwa kuwa ushahidi upo, anaamini Morocco watachukuliwa hatua.Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe alishauri Stars icheze chini ya angalizo kwa kuwasilisha barua FIFA mapema ili wakae wanajua kuhusu hali halisi Morocco.Kwa ujumla kilichotokea leo kimewatia woga Watanzania wengi waliopo hapa kuelekea mchezo wa kesho, ambao Stars inahitaji ushindi ili kujiimarisha katika mbio za kuelekea Brazil 2014. Hata ulinzi wa msafara wa Stars kutoka hotelini hadi uwanjani hakuwa wa kutosha na ilishuhuidiwa mara kadhaa ukiingiliwa na magari mengine barabarani wakati timu ikienda uwanjani kwa mazoezi.Wenyeji nchini Morocco wanasema inapowadia mechi, huwa wanaogopa kwa sababu mara nyingi hutokea vurugu ya damu kumwagika.Kwa ujumla Stars inaingia katika mchezo wa kesho katika hali ya wasiwasi na woga mkubwa. Stars itashuka dimbani saa 3:00 usiku kesho kwa saa za hapa sawa na saa 5:00 za Tanzania kucheza na Morocco.Stars inashika nafasi ya pili katika Kundi C, ikiwa na pointi sita nyuma ya Ivory Coast yenye pointi saba, ambayo kesho itakuwa ugenini ikimenyana na Gambia katika mchezo mwingine wa kundi hilo.

Stars ilitua hapa Jumatatu ikitokea Ethiopia ambako iliweka kambi ya wiki moja na kucheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Sudan, ulioisha kwa sare ya bila mabao.Kabla ya kuja hapa, Stars iliweka kambi ya wiki moja katika hoteli ya Tansoma, Dar es Salaam ikijifua Uwanja wa Karume na siku chache kabla ya kuondoka ilialikwa Ikulu na Rais Jakaya Kikwete, aliyewapa hamasa kwa hotuba nzuri.

No comments:
Post a Comment